Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mussa Azan Zungu, akifungua Semina ya kuwajengea uwezo Wabunge Wanawake kuhusu Mradi wa kusambaza nishati safi na salama ya kupikia vijijini, iliyofanyika Dodoma, Septemba 22, 2022. Semina hiyo iliandaliwa na REA.
Mkurugenzi wa Uendelezaji Masoko na Teknolojia kutoka Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Advera Mwijage akiwasilisha Mada wakati wa Semina ya kuwajengea uwezo Wabunge Wanawake kuhusu Mradi wa kusambaza nishati safi na salama ya kupikia vijijini, iliyofanyika Dodoma, Septemba 22, 2022. Semina hiyo iliandaliwa na REA.
Sehemu ya Wajumbe wa Menejimenti na Wafanyakazi wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) wakifuatilia Semina ya kuwajengea uwezo Wabunge Wanawake kuhusu Mradi wa kusambaza nishati safi na salama ya kupikia vijijini, iliyofanyika Dodoma.
Na Issa Sabuni - REA
WAKALA wa Nishati Vijijini (REA) umeendesha Semina ya kuwajengea uwezo
Wabunge Wanawake kuhusu Mradi wa kusambaza nishati safi na salama ya kupikia
vijijini.
Akifungua Semina hiyo iliyofanyika Dodoma, Septemba 22 mwaka huu, Naibu
Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mussa Azan Zungu
aliwahamasisha Washiriki kuwa mfano kwa wananchi katika maeneo yao, namna gani
wanaweza kupikia nishati ambayo ni salama.
“Tuzingatie na tusaidiane kupeleka nishati mbadala kwenye maeneo yetu na
hasa sisi wabunge, tuanze kuonesha mfano.”
Aidha, alizungumzia suala la uchafuzi wa mazingira unaosababishwa na
ukataji miti kwa ajili ya kuni na mkaa ambapo alisema pamoja na mambo mengine,
umeathiri Mlima Kilimanjaro ambacho ni kivutio cha utalii nchini.
Akifafanua, alisema utafiti unaonesha kuwa hewa ya moto ambayo hupaswa
kupozwa na miti hususan katika mikoa ya Pwani, Dar es Salaam na Tanga,
inakwenda kwenye Mlima Kilimanjaro jambo linalochangia kupoteza barafu yake.
Naibu Spika alisisitiza kuwa Wabunge Wanawake wana nafasi kubwa ya kuleta
mabadiliko chanya kwenye eneo la nishati safi na salama na kuokoa afya za
watumiaji wa kuni na mkaa hususan akina mama na watoto.
“Tumeambiwa na Wataalam kuwa Mama akipika kwenye moshi kwa saa moja ni sawa
na kuvuta sigara mia tatu. Kwa hali hii atakuwa ameathirika kwa kiwango kikubwa
na kwa wenye ujauzito itamuathiri hata mtoto aliye tumboni.”
Kwa upande wake, Waziri wa Nishati, Mhe. January Makamba, akizungumza
kupitia video fupi iliyorekodiwa na kuchezwa katika Semina hiyo, aliomba
ushirikiano kutoka kwa Wabunge Wanawake katika kufanikisha mkakati huo maalum
unaotekelezwa na Wizara kupitia REA, ili kuleta mapinduzi katika nishati ya kupikia
hususan vijijini.
Waziri Makamba ambaye hakuweza kushiriki katika Semina husika kutokana na
majukumu mengine ya kitaifa, alibainisha kupitia video hiyo fupi kuwa athari za
matumizi ya kuni na mkaa ni kubwa hasa kwa akina mama na watoto lakini hazisemwi
sana kwani kundi linaloathirika zaidi halina sauti.
Akitoa takwimu, alisema kuwa utafiti unaonesha takribani watu 33,000
hupoteza maisha kila mwaka hapa nchini kutokana na kuvuta hewa ya ukaa
inayosababishwa na matumizi ya kuni na mkaa katika kupikia.
Alisema kuwa kutokana na madhara makubwa yanayosababishwa na matumizi ya
nishati zisizo salama, Wizara kupitia REA imeamua kuweka juhudi za makusudi
kuhakikisha inawakomboa akina mama hususan waishio vijijini kutoka katika
madhara ya kiafya pamoja na kupunguza athari kwa mazingira.
Akizungumza katika Semina hiyo, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya
Nishati na Madini, Mhe. Dunstan Kitandula, alipongeza kazi kubwa iliyofanywa na
REA katika kupeleka nishati ya umeme vijijini na kuongeza kuwa kazi ya kuhamasisha
matumizi ya nishati mbadala kwa kupikia vijijini ni kubwa zaidi hivyo Wakala
unapaswa kuungwa mkono katika utekelezaji wake.
“Kwahiyo Wabunge wenzangu, tulichukue jambo hili, tulisemee kwa nguvu kubwa
kwa umoja wetu ili tuweze kupata matokeo chanya ambayo wote tunayatarajia,”
alisisitiza.
Mwakilishi wa Wizara ya Nishati katika Semina hiyo, Mhandisi Edson Ngabo
alisema kuwa katika kuhakikisha upatikanaji wa nishati bora ya kupikia,
Serikali imeanza utekelezaji awamu kwa awamu ambapo katika Mwaka huu wa Fedha
(2022/23) Shilingi Bilioni Tano zimetengwa kwa ajili ya kusambaza gesi asilia
kwa ajili ya kupikia katika mikoa ya Pwani na Dar es Salaam.
Awali, akitoa salamu za Ukaribisho, Mwenyeji wa Semina hiyo, Mkurugenzi
Mkuu wa REA, Mhandisi Hassan Saidy, alisema kuwa, kwa kutambua kwamba kuna
madhara ya kuendelea kutumia nishati isiyo salama, Serikali imekuja na Mpango
Maalum wa kuwezesha upatikanaji wa nishati bora ya kupikia vijijini.
Alieleza zaidi kuwa, katika Mpango huo, kuna maeneo kadhaa ya kipaumbele
ikiwemo kujenga ufahamu, hasa kwa wananchi kuhusu upatikanaji na kuhamasisha
matumizi ya bidhaa na teknolojia za nishati bora vijijini.
Mkurugenzi Mkuu alifafanua kuwa, baadhi ya watu hawafahamu kama kuna majiko
hivi sasa yanayotumia kiwango cha nishati inayotumika kupikia mlo mmoja na
kutumia kiwango kilekile kupikia mlo zaidi ya mmoja.”
“Kwahiyo, tutawajengea ufahamu kuhusu upatikanaji wake na kuhamasisha pia
matumizi yake, tukiwalenga zaidi wananchi wa vijijini,” alibainisha Mhandisi
Saidy.
Akiwasilisha Mada katika Semina hiyo, Mkurugenzi wa Uendelezaji Masoko na
Teknolojia kutoka REA, Mhandisi Advera Mwijage, alitaja baadhi ya madhara
yatokanayo na matumizi ya nishati isiyo bora na salama kwa kupikia kuwa ni
pamoja na kupoteza nguvu kazi ya Taifa.
Mhandisi Mwijage alibainisha kuwa vifo vitokanavyo na uvutaji wa hewa ya
ukaa majumbani ni asilimia 8.5.
Semina hiyo kwa Wabunge Wanawake ilihudhuriwa pia na Wenyeviti wa Kamati za
Kudumu za Bunge, Wabunge Vinara, Menejimenti ya REA, Mwakilishi kutoka TPDC pamoja
na Wadau mbalimbali wanaojishughulisha na uendelezaji wa teknolojia mbadala za
nishati ya kupikia.