Sunday, December 10, 2023

SERIKALI YATOA MIL. 114/- KITUO CHA AFYA MTAE, MSD YAKIKABIDHI VIFAA TIBA

Afisa Huduma kwa Wateja wa Bohari ya Dawa (MSD) Kanda ya Tanga, Mary Isango, akimpatia nyaraka mbalimbali, Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya cha Kijiji cha Mtae kilichopo Lushoto mkoani Tanga, Shafii Makamba (kulia), wakati wa makabidhiano ya vifaa tiba vyenye thamani ya Sh.Milioni 114 zilizotolewa na Serikali kwa ajili ya kununulia vifaa hivyo kupitia MSD kwenye tukio la makabidhiano lililofanyika Disemba 9, 2023. Wengine wanaoshuhudia tukio hilo kutoka kushoto ni Dereva wa MSD, Rashidi Msambo na Mwenyekiti wa Kijiji cha Mtae, Andrew Kilama. 

.........................................................

Na Dotto Mwaibale, Lushoto

SERIKALI imetoa Sh.Milioni 114 kwa Kituo cha Afya  Mtae kilichopo Wilaya ya Lushoto mkoani Tanga ambazo zimetumika kununulia vifaa tiba kupitia Bohari ya Dawa (MSD) na hivyo kinatarajia kuanza kutoa huduma ya upasuaji mwishoni mwa mwezi Disemba 2023.

Hatua ya kituo hicho kuanza  kutoa huduma hiyo inatokana na maboresho makubwa yaliyofanywa na Serikali ya kuibadilisha zahanati ya kijiji cha Mtae kuwa Kituo cha  Afya ili wananchi waweze kupata huduma bora na karibu.

Mganga Mfawidhi wa kituo hicho,  Shafii Makamba akizungumza wakati akipokea vifaa hivyo kutoka MSD alianza kwa kuishukuru Serikali inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassani kupitia MSD kwa kuwezesha kutoa vifaa hivyo vya dharura kwa ajili ya kufanya huduma ya dharura kwa wakina mama na watoto.

"Vifaa hivi tulivyovipokea leo kutoka MSD Kanda ya Tanga  vitasaidia kupunguza vifo vya wajawazito na watoto kwa sababu kabla ya hapo walikuwa wakilazimika kutembea umbali usiopungua kilometa 65 kwenda Hospitali ya Wilaya ya Lushoto kupata huduma za dharura hasa za upasuaji na kuwa wataachana na adha hiyo na kupata huduma hii hapa hapa katika kituo chetu," alisema Makamba.

Afisa Huduma kwa Wateja wa MSD Kanda ya Tanga, Mary Isango akizungumza wakati akikabidhi vifaa hivyo kwa niaba ya Meneja wa MSD wa kanda hiyo, Sitti Abdulrahman, alisema wamepeleka vifaa hivyo baada ya kituo hicho cha afya kujengwa jengo la upasuaji na kupelekewa vifaa hivyo vyenye thamani ya Sh.Milioni 114 ambavyo vinaenda kuondoa changamoto waliyokuwa wakiipata wananchi kwenda kupata huduma hiyo mbali.

"Huduma za upasuaji sasa zitafanyika katika kituo hiki baada ya kupata vifaa hivi ambavyo ni muhimu sana sisi kama bohari ya dawa wito wetu kwa watendaji wa kituo hiki ni kuvitunza ili viweze kudumu muda mrefu na kuleta tija kwa wananchi kadri watakavyokuwa wakiendelea kuvitumia kwa kuzingatia kuwa Serikali imekuwa ikitumia fedha nyingi kuvinunua," alisema Isango.

Baadhi ya wakazi wa Kijiji cha Mtae, Beatrice Alphonce, Disifa Mdoe na Mwenyekiti wa Kijiji hicho, Andrew Kilama waliishukuru Serikali kupitia MSD kwa kuwapelekea vifaa hivyo ambavyo vitaondoa kabisa madhira waliyokuwa wakiyapata na wakati mwingine kusababisha vifo.

"Tulikuwa na changamoto kubwa baadhi ya wajawazito walikuwa wakijifungulia njiani kutokana na umbali mrefu wa kwenda Hospitali ya Wilaya ya Lushoto kupata huduma lakini sasa tutakuwa tunaipata hapahapa nyumbani kwa kweli tuna kila sababu ya kumshukuru Rais wetu mama Samia kwa kutuona na kutuonea huruma wanawake wenzake na kama ingewezekana tungemuomba siku moja aje hayaone kwa macho maendeleo haya aliyotuletea," alisema Alphonce.

Alphonce alitumia nafasi hiyo kumshukuru Rais Samia, Mbunge wa jimbo hilo, Rashid Shangazi na viongozi wa wilaya hiyo kwa jitihada kubwa wanayoifanya ya kuwaletea maendeleo hayo ambapo aliwaombea kwa Mungu awape afya na maisha marefu.Afisa Huduma kwa Wateja wa Bohari ya Dawa (MSD) Kanda ya Tanga, Mary Isango na Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya cha Kijiji cha Mtae, Shafii Makamba wakizipitia nyaraka hizo kabla ya kukabidhiana vifaa hivyo.Mapitio ya nyaraka hizo yakifanyika kwa pamoja kabla ya makabidhiano. Kutoka kushoto ni Afisa Huduma kwa Wateja wa Bohari ya Dawa (MSD) Kanda ya Tanga, Mary Isango, Dereva wa MSD, Rashidi Msambo, Mwenyekiti wa Kijiji cha Mtae, Andrew Kilama na  Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya cha Kijiji cha Mtae, Shafii Makamba,Mwenyekiti wa Kijiji cha Mtae, Andrew Kilama akishukuru Serikali kwa kuwapelekea vifaa hivyo kupitia MSD,Muonekano wa Zahanati ya Kijiji cha Mtae kabla ya kubadilishwa kuwa Kituo cha AfyaMuonekano wa jengo la upasuaji lililojengwa na Serikali na kuipandisha hadhi zahanati hiyo kuwa Kituo cha Afya.Vifaa tiba hivyo vikitolewa kwenye gari tayari kwa makabidhiano.Vifaa tiba vikipelekwa kwenye jengo la upasuaji.Watoto wa Kijiji hicho wakishiriki kubeba vifaa hivyo.Kazi ya ubebaji wa vifaa hivyo ikiendelea.Vifaa vikibebwa.Wananchi wa kijiji hicho wakishiriki kubeba vifaa hivyo.Mkazi wa kijiji hicho, Beatrice Alphonce akiishukuru Serikali na MSD kwa kufanikisha kupatikana kwa vifaa hivyo.Mkazi wa kijiji hicho, Disifa Mdoe akipipongeza Serikali na MSD kwa kuwapelekea vifaa hivyo.Gari la MSD likiwa safarini kupeleka vifaa hivyo.

Monday, December 4, 2023

REA YAWASHA MRADI WA BILIONI 25 KUPOZA, KUSAMBAZA UMEME IFAKARA MOROGORO

Mkuu wa Wilaya ya Kilombero, Mhe. Dunstan Kyobya, akizungumza baada ya kuwasha  Kituo cha Kupoza na Kusambaza Umeme cha Ifakara    (Ifakara Substation), Desemba 3, 2023 Ifakara, Morogoro. Kituo kimejengwa na Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kwa kushirikiana na Umoja wa Ulaya (EU) kwa gharama ya Shilingi bilioni 25.

...........................................................................

Na Mwandishi Wetu, Ifakara-Morogoro

SERIKALI  ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kwa kushirikiana na Umoja wa Ulaya (EU) imewasha Kituo cha Kupoza na Kusambaza Umeme cha  Ifakara ambacho kimegharimu shilling bilioni 25.

Akiwasha kituo hicho ambacho kimelenga kuongeza uwekezaji na uanzishaji wa viwanda kwa upatikanaji wa umeme wa uhakika, Mkuu wa Wilaya ya Kilombero , Mh Dunstan Kyobya ameshauri kituo hicho kiitwe Samia Ifakara Substation.

Ameipongeza REA na EU kwa kuhakikisha kituo kimekamilika na kuwashwa kwani kinaenda kumaliza matatizo ya umeme katika wilaya ya Kilombero, Malinyi na Ulanga ambayo ni maeneo ya kimkakati ya kilimo na viwanda.

“Tunategemea kuongeza uwekezaji kwa kuanzisha viwanda vya kuongeza thamani ya mazao ya kilimo na vile vya kuchakata madini” amesema Mh Kyobya.

Amewataka wananchi kuhakikisha wanatunza mazingira na vyanzo vya maji ili kujihakikishia umeme wa uhakika katika mabwawa ya kuzalisha umeme ya Kihansi na Kidatu.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa REA, Mhandisi Jones Olotu amesema kuwashwa kwa kituo hicho kunaongeza upatikanaji wa umeme na hivyo kuwawezesha wananchi  kukuza na kuboresha hali zao za kiuchumi kwa kufungua biashara mbalimbali kwa uwepo wa umeme wa uhakika katika maeneo hayo.

“Wananchi watumie upatikanaji wa umeme wa uhakika kwa kujiongezea kipato kwa kuwekeza na kuanzisha viwanda vya mazao ya kilimo na madini ambayo yanapatikana kwa wingi Kilombero, Ifakara, Ulanga na Malinyi,” amesema Mhandisi Olotu.

Naye Mbunge wa Kilombero, Aboubakar Asenga amewataka wananchi wa Jimbo hilo kuchangamkia fursa ya upatikanaji wa umeme mkubwa kwa kuzalisha kwa wingi na kuanzisha viwanda vikubwa.

“Tunaishukuru serikali kwa kutimiza ahadi yake, ni wajibu wetu wananchi kutumia fursa hii ya upatikanaji wa umeme mkubwa kwa kuwa na viwanda vya kukausha na kukoboa mpunga, uzalishaji wa matofali kwa kisasa na uongezaji thamani wa madini ili kujiongezea kipato, ” amesema Mh Asenga.

Meneja wa Mradi huo kutoka REA, Mhandisi Romanus Lwena amesema ujenzi wa kituo hicho ulianza 2020 ambapo kinazalisha kV 220 za umeme baada ya wananchi wa maeneo hayo kuwa wanapata umeme mdogo wa kV 33 uliokuwa unasababisha kukatika mara kwa mara.

Na baada ya kuwashwa kwa kituo hicho, kutawezesha kuwa na umeme wa uhakika kwa ajili ya viwanda na shughuli nyingine za kilimo.

Meneja Miradi ya Nishati wa EU, Mhandisi Francis Songela amesema katika Mradi huo wamechangia shilingi bilioni 18 na Serikali ya Tanzania imetoa shilingi bilioni 7.

Amesema kituo hicho kipo katika eneo la  kimkakati la  Mpango wa Kukuza Kilimo Ukanda wa Kusini mwa Tanzania , SAGCOT ambapo Mradi huo unaenda kuleta mapinduzi ya kilimo na viwanda.

“Wilaya za Kilombero, Ulanga na Malinyi ni maeneo ya kimkakati ya SAGCOT kwani yana rutuba kwa kilimo na shughuli nyingi za kiuchumi ambapo umeme wa uhakika ilikuwa changamoto  na kwa kuwashwa kwa kituo hiki tunategemea mapinduzi ya kilimo na viwanda, ” amesema Mhandisi Songela.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Jones Olotu akizungumza.
. Mbunge wa Kilombero, Mhe. Aboubakar Asenga akizungumza.
 Meneja wa Mradi wa Ujenzi wa Kituo cha Kupoza na Kusambaza Umeme cha Ifakara (Ifakara Substation) kutoka Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Romanus Lwena akitoa maelezo kuhusu Kituo hicho kwa Mkuu wa Wilaya ya Kilombero, Mhe. Dunstan Kyobya na Viongozi wengine mbalimbali wakati wa tukio la kuwasha Kituo hicho kilichojengwa na Serikali kupitia REA kwa kushirikiana na Umoja wa Ulaya (EU) kwa lengo la kuimarisha huduma ya upatikanaji umeme kwa wananchi wa wilaya za Kilombero, Ulanga na Malinyi.
Taswira ya Kituo cha Kupoza na Kusambaza Umeme cha Ifakara (Ifakara Substation). Taswira hii ilichukuliwa Desemba 3, 2023 wakati wa tukio la kuwasha rasmi Kituo hicho baada ya ujenzi wake kukamilika.
Mkuu wa Wilaya ya Kilombero, Mhe. Dunstan Kyobya (katikati)  akiwa pamoja na Viongozi mbalimbali na wataalam kutoka Wakala wa Nishati Vijijini (REA), TANESCO na Umoja wa Ulaya (EU) wakifurahi baada ya tukio la kuwasha rasmi Kituo cha Kupoza na Kusambaza Umeme cha Ifakara (Ifakara Substation), Desemba 03, 2023.

Sunday, November 26, 2023

BOHARI YA DAWA (MSD) YATWAA TUZO YA MLIPA KODI BORA 2023

 Mkurugenzi Mkuu wa MSD, Mavere Tukai (kushoto) akipokea tuzo ya mlipa kodi bora.

MSD Yatwaa Tuzo Ya Mlipakodi Bora 2023

..............................................

 

Na Mwandishi Wetu


BOHARI ya Dawa (MSD), imetwaa tuzo ya Mlipakodi Bora kwa mwaka 2023 ya Mamlaka ya Kodi Tanzania.

Tuzo hizo zimetolewa  usiku wa Novemba 24, 2023 katika hafla maalum ya wiki ya Mlipakodi zilizofanyika katika Ukumbi wa Mlimani City jijiini Dar es Salaam ambako Bohari hiyo imeibuka mshindi wa kwanza katika kipengele cha WalipakodiWalipakodi wa Kati kwa Mkoa wa Kikodi wa Temeke.

Akipokea tuzo hiyo, Mkurugenzi Mkuu wa MSD, Mavere Tukai amesema ushindi huo una maana kubwa kwa Bohari hiyo na Watanzania.

Amesema MSD ambayo ni moja ya Taasisi za kimkakati za Serikali inayohusika na kuzalisha, kununua, kutunza na kusambaza bidhaa za afya kwa ajili ya vituo vya kutolea huduma za afya vya Serikali nchini inafuata taratibu, sheria na miongozose ikiwa ni pamoja na kulipa kodi stahiki.

"Maendeleo yoyote ya nchi yanategemea kodi zinazolipwa hivyo ni vyema kila mlipa kodi akalipa kodi stahiki ili kuwezesha muendelezo wa biashara na  kuimarisha maendeleo kwa mustakali wa ustawi wa jamii, " ameongeza Tukai katika hafla hiyo ambako mgeni Rasmi alikuwa Naibu Waziri Mkuu, Dk Dotto Biteko.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi Tukai, MSD sasa iko katika mkakati wa kujiendesha kibiashara hivyo hatua ya kulipa kodi kwa utaratibu uliowekwa hadi kutambuliwa ni fursa ya kuaminika kwa wadau wetu katika huduma tunazotoa.

Awali Mkurugenzi wa Elimu wa Mlipakodi na Mawasiliano, Richard Kayombo alisema vigezo vilivyotumika kupata washindi ni kulipa kiasi kikubwa cha kodi na hiari pamoja na kutunza kumbukumbu vizuri

Tuzo hiyo ya mlipa kodi bora ikioneshwa.
 

Tuesday, November 21, 2023

SERIKALI YAMWAGA VIFAA TIBA VYA SH. MILIONI 222.472 SINGIDA

 

  Meneja  wa  Bohari ya Dawa  (MSD) Kanda ya Dodoma Mwanashehe Jumaa (katikati kulia) akipeana mkono na Mbunge wa Jimbo la Singida, Mashariki, Miraji Mtaturu  ikiwa ni ishara ya kumkabidhi jenereta na vifaa tiba vilivyotolewa na Serikali kupitia MSD kwenye hafla iliyofanyika Novemba 20,2023 katika Hospitali ya Wilaya ya Ikungi.

.................................................

Na Dotto Mwaibale, Singida

SERIKALI  ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kupitia Bohari ya Dawa (MSD) imekabidhi vifaa tiba Mkoa wa Singida vyenye jumla ya takribani Sh.Milioni 222.472.

Vifaa hivyo ni pamoja na majenereta, sambamba na vifaa vitakavyotumika kuhudumia watoto wanaozaliwa kabla ya muda na huduma nyinginezo ambavyo vimekabidhiwa kwenye Hospitali ya Wilaya ya Ikungi, Kituo cha Afya Sepuka na Hospitali ya Wilaya ya Singida, Ilongero.

Akizungumza kwenye hafla ya kukabidhi vifaa hivyo ambayo ilishuhudiwa na wabunge, watendaji wa idara mbalimbali za sekta ya afya, wananchi pamoja na Wanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) , Meneja  wa MSD Kanda ya Dodoma Mwanashehe Jumaa alisema kazi hiyo ya usambazaji wa vifaa hivyo ni jukumu lao walilopewa na Serikali.

" Kazi yetu kubwa sisi MSD ni Uzalishaji, Ununuzi,  Uhifadhi na Usambazaji wa  bidhaa za afya na vitendanishi hapa nchini ambayo tunaifanya kwa mamlaka ya kisheria," alisema Jumaa.

“MSD leo tupo hapa Ikungi kwa ajili ya kukabidhi jenereta, kitanda cha kufanyia upasuaji, Ultra-Sound mashine pamoja na mashine ya kuasaidia kuwapatia joto watoto wachanga na waliozaliwa kabla ya wakati.(njiti-Infant Radlant warmer) vyenye thamani ya zaidi ya Sh.Milioni 72

Jumaa alisema lengo kubwa la kupelekwa kwa vifaa hivyo ni kuhakikisha huduma za uzazi zinaboreshwa na kuwa katika wilaya hiyo MSD ilikuwa inakamilisha vifaa ambavyo ilikuwa imepokea fedha zaidi ya Sh. Milioni 300 ili kukamilisha usambaji wake.

Alisema MSD Kanda ya Dodoma imepokea maombi  ya vifaa  tiba zaidi ya  700  Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi kwa ajili ya vituo  vya Afya  na Zahanati.

"Ukiangalia muda tuliopokea fedha hizi na utekelezaji wa kupeleka vifaa hivyo ni muda mfupi sana na hiyo imetokana na Serikali kuboresha huduma za MSD na kufikia hatua hii ya kukamilisha vifaa ambavyo hatukuvipeleka awali na kuvipeleka sasa baada ya fedha zake kuzipokea muda mfupi uliopita," alisema Jumaa.

Alisema Serikali imekuwa ikitoa fedha na MSD imekuwa ikinunua na kusambaza vifaa tiba katika hospitali na vituo vya afya kote nchini ambapo aliishukuru kwa hatua hiyo na kueleza kuwa inajenga morali kwa watumishi wa sekta ya afya na kuipenda kazi wanayoifanya.

Mbunge wa Jimbo la Singida Mashariki Miraji Mtaturu  aliishuru Serikali na MSD kwa kupeleka vifaa hivyo na kueleza kuwa sekta ya afya ni uhai na kuwa watu wakiwa na afya njema ndipo wataweza kufanya kazi zao vizuri.

"Leo hii tunashuhudia vifaa hivi vilivyo letwa na Serikali kupitia MSD na kukabidhi hospitali yetu ya Ikungi maana yake ni utekelezaji wetu wa kujenga Hospitali ya Wilaya ambayo tuliiomba kwa muda mrefu," alisema Mtaturu.

Alisema kujenga majengo tu ya hospitali haitoshi na kuwa inahitaji na vitu vya ziada vikiwemo vifaa na kuwa madaktari na wataalamu wengine wamesomeshwa kwa lengo la kuwasaidia watu kutibu maradhi mbalimbali na kwa kuvitumia vifaa hivyo ndio wanaweza kufanya kazi yao kwa urahisi iwe kwa kupima na kufanya upasuaji.

Mtaturu alisema Serikali chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imefanya mapinduzi makubwa sana katika sekta ya afya hapa nchini hivyo kila mtu mpenda maendeleo anapaswa kumshukuru kwa jinsi anavyo iendesha nchi kwenye sekta mbalimbali.

Mbunge wa Jimbo la Singida Magharibi, Elibariki Kingu akipokea vifaa hivyo kwa ajili ya Kituo cha Afya cha  Sepuka alisema miongoni mwa vifaa alivyo pokea kutoka MSD ni jenereta lenye ukubwa wa KVA 60 na vifaa vingine 11 ambavyo baadhi ni toroli la kuwekea vifaa wakati madaktari na wauguzi wanapokwenda kutoa huduma, vifaa vinavyotumika kumsaidia mtoto baada ya kuzaliwa aweze kupumua vizuri na kuwa vifaa vyote alivyovipokea vinatumika kupingana na uzazi pingamizi na lengo lake ni kumuokoa mama wala mtoto wasife wakati wa kujifungua.

Alitaja vifaa vingine alivyopokea ni mashine kwa ajili ya hewa, mashine ya kupimia uzito, kifaa cha kutundikia dripu ya maji, kifaa cha kuwapa joto watoto waliozaliwa kabla ya muda, kifaa cha kuvuta uchafu kwenye njia ya hewa baada ya mtoto kuzaliwa, saa ya ukutani, kifaa kinachobeba vifaa vya kumuhudumia mtu aliyepata majeraha na pampu inayotumika kumnyonya mtoto kwa ajili ya kuondoa kitu kilichokwama kooni au kupoteza fahamu baada ya kupaliwa na kuwa vifaa hivyo vyote vina thamani ya zaidi ya Sh.Milioni 82.

Kingu aliishukuru Serikali kwa kutoa fedha na akapongeza maboresho makubwa yaliyofanywa ndani ya MSD na kueleza kuwa MSD ya leo ni ya kisasa na mkombozi kwa wananchi katika kazi ya kutoa huduma za afya si kwa Mkoa wa Singida pekee bali kwa nchi nzima kazi ambazo zimekuwa zikionekana kupitia vyombo vya habari.

Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Singida Kaskazini, Ramadhani Ighondo aliishukuru Serikali kwa kuwapelekea jenereta na gari la kuwabebea wagonjwa na wajawazito ambao wengi wao walikuwa wakipoteza maisha kutokana na kukosa umeme wa uhakika wakati wakipata huduma hasa za upasuaji na kukosekana kwa gari la kuwapeleka hosptali wanapokuwa wagonjwa.

Ighondo alisema pamoja na kupelekewa gari hilo pia Serikali kupitia MSD imewapelekea kifaa kinachotumika kwa ajili ya kuwaongezea joto watoto wanaozaliwa chini ya muda.

Alisema mbali ya gari hilo la wagonjwa vifaa walivyopokea vina thamani ya zaidi ya Sh.Milioni 62.7

Mganga Mkuu wa Wilaya ya Ikungi, Dorisila Mlenga, Mganga Mkuu wa Wilaya ya Singida, Grace Ntogwisangu pamoja na Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya Sepuka, Kesia Daniel waliishukuru Serikali kwa kuwapelekea vifaa hivyo ambavyo vinakwenda kuwarahisishia utendaji wa kazi za kutoa huduma kwa wananchi ambapo walisema watavisimamia na kuvitunza ili viweze kudumu kwa muda mrefu wakizingatia Serikali imekuwa ikitumia fedha nyingi kuvinunua.

Wananchi Elesisia Mlenga, Asha Salim, Asha Musa, Mwalimu Tatu Njoka, Ashura Iddi na Mwanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Seketoure, Getruda Yona waliishukuru Serikali kupitia MSD kwa kuwapekea jenereta na gari la wagonjwa na kueleza kuwa vifaa hivyo vinakwenda kuwasaidia katika kupata huduma bora za afya.

Mwanafunzi Getruda Yona alimshukuru Rais Samia kwa kuwajengea shule na kuwapunguzia umbali mrefu ambapo walikuwa wakitembea zaidi ya kilomita 10 kwenda shuleni kabla ya kujengewa kwa shule hiyo ya Seketoure.

Meneja  wa  Bohari ya Dawa  (MSD) Kanda ya Dodoma Mwanashehe Jumaa (katikati kulia) akipeana mkono na Mbunge wa Jimbo la Singida Magharibi, Elibariki Kingu  ikiwa ni ishara ya kumkabidhi jenereta na vifaa tiba vilivyotolewa na Serikali kupitia MSD kwenye hafla iliyofanyika Novemba 20,2023 katika Kituo cha Afya cha Sepuka Wilaya ya Ikungi. Kutoka kushoto ni Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya Sepuka, Kesia Daniel , Diwani wa Kata ya Sepuka Halima Ng'imba, Afisa Huduma Mwandamizi kwa Wateja MSD Kanda ya Kati, Juliana Mbogo na  Mfamasia wa Kanda na Afisa Huduma kwa Wateja MSD Kanda ya Kati Dodoma, Michael Mwakuna.


Meneja  wa  Bohari ya Dawa  (MSD) Kanda ya Dodoma Mwanashehe Jumaa (katikati kushoto) akipeana mkono na Mbunge wa Jimbo la Singida Kaskazini, Ramadhani Ighondo ikiwa ni ishara ya kumkabidhi jenereta na vifaa tiba vilivyotolewa na Serikali kupitia MSD kwenye hafla iliyofanyika Novemba 20,2023 katika Hospitali ya Wilaya ya Singida.

Meneja  wa  Bohari ya Dawa  (MSD) Kanda ya Dodoma Mwanashehe Jumaa (katikati kulia) akisisitiza jambo wakati wa kukabidhi vifaa hivyo kwa Mbunge wa Jimbo la Singida, Magharibi Elibariki Kingu (kushoto) Kulia ni Afisa Huduma kwa Wateja Mwandamizi wa MSD Kanda ya Kati, Juliana Mbogo.

Meneja  wa  Bohari ya Dawa  (MSD) Kanda ya Dodoma Mwanashehe Jumaa, akipeana mkono na Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya cha Sepuka Kesia Daniel baada ya kukabidhi vifaa hivyo.

Meneja  wa  Bohari ya Dawa  (MSD) Kanda ya Dodoma Mwanashehe Jumaa, akiwa katika picha ya pamoja na Wafanyakazi wa MSD na wakituo cha Afya cha Sepuka baada ya kukabidhi vifaa tiba hivyo.

Meneja  wa  Bohari ya Dawa  (MSD) Kanda ya Dodoma Mwanashehe Jumaa, akizungumza na wakazi wa Wilaya ya Singida wakati wa kukabidhi vifaa hivyo
Mbunge Ramadhani Ighondo akizungumza na wananchi wakati wa hafla hiyo.

Mganga wa Wilaya ya Singida, Grace Ntogwisangu, akizungumza na wananchi kwenye hafla hiyo.
Gari la MSD , likiwa tayari kushusha vifaa hivyo.
Meneja  wa  Bohari ya Dawa  (MSD) Kanda ya Dodoma Mwanashehe Jumaa (katikati) na Afisa Huduma Mwandamizi kwa Wateja wa NSD, Juliana Mbogo wakiwajibika wakati wa kukabidhi vifaa hivyo.
Mbunge wa Jimbo la Singida Magharibi, Elibariki Kingu, akizungumza na wananchi wa Kata ya Sepuka wakati wa kupokea vifaa hivyo.

Mbunge wa Jimbo la Singida Magharibi, Elibariki Kingu,Meneja  wa  Bohari ya Dawa  (MSD) Kanda ya Dodoma Mwanashehe Jumaa na Afisa Huduma Mwandamizi kwa Wateja wa MSD, Juliana Mbogo wakiwa na zawadi zao za kuku walizopewa na Wanawake wa Kata ya Sepuka.
Wananchi wa Kata ya Sepuka wakiwa kwenye hafla ya kupokea vifaa hivyo.

Meneja  wa  Bohari ya Dawa  (MSD) Kanda ya Dodoma Mwanashehe Jumaa, akiwa katika picha ya pamoja na wanawake waliohudhuria kliniki wakati wa makabidhiano ya vifaa hvyo Kata ya Sepuka.

Muonekana wa moja ya magenereta yaliyo kabidhiwa na MSD katika Hospitali ya Wilaya ya Ikungi, Singida na Kituo cha Afya cha Sepuka.
Wanawake wakiwa kwenye hafla ya kukabidhiwa vifaa hivyo Hospitali ya Wilaya ya Singida, Ilongero. 


Wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Seketoure wakiwa kwenye hafla hiyo.

Diwani wa Kata ya Ilongero, Issa Mwiru akizungumza na wananchi wakati wa hafla hiyo.

Gari la wagonjwa lililotolewa na SAerikali kwa ajili ya Halmashauri ya Wilaya ya Singida likioneshwa kwa wananchi (hawapo pichani) wakati wa hafla hiyo ya kupokea vifaa tiba.

Diwani wa Viti Maalumu wa Kata ya Ilongero, Mwanamoshi Bakari, akizungumza kwenye hafla hiyo.

Muonekano wa baadhi ya majengo ya Hosptali ya Wilaya ya Ikungi.

Muonekano wa moja la jengo la Kituo cha Afya cha Sepuka.

Muonekano wa moja ya jengo la Hospitali ya Wilaya ya Singida Ilongero.
Jenereta likiwa limebebwa kwa jeki tayari ya kuhifadhi katika Hospitali ya Wilaya ya Ikungi wakati ikisubiriwa kujenga kibanda litakalo wekwa.


Sunday, November 19, 2023

WAHITIMU WANAWAKE WANG'ARA MAHAFALI YA 21 TAASISI YA UHASIBU SINGIDA

 

Mkuu wa Wilaya ya Iramba Suleimani Mwenda (katikati) akiongoza maandamano ya wahitimu wa Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA) Kampasi ya Singida wakati wakiwasili kwenye mahafali ya 21 ya taasisi hiyo yaliyofanyika Novemba 17, 2023. Kulia kwake ni Wakili Said Chuguma ambaye ni Mwenyekiti wa Bodi ya Ushauri ya Wizara ya Fedha na kushoto ni Afisa Mtendaji Mkuu (CEO) wa Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA), Profesa William Pallangyo.

Na Dotto Mwaibale, Singida

SHEREHE za Mahafali ya 21 ya Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA) Kampasi ya Singida imemalizika huku idadi kubwa ya wanawake  ikizidi kuongezeka mara dufu ikilinganishwa na idadi ya wanaume.

Kwa mujibu wa taarifa ya taasisi hiyo jumla ya wanawake 938 sawa na asilimia 55.2 wamehitimu katika mahafali hayo Kampasi ya Singida ikilinganishwa na idadi ya wanaume 762 sawa na asilimia 44.8.

Akizungumza kwenye mahafali hayo yaliyofanyika Novemba 17, 2023 Afisa Mtendaji Mkuu (CEO) wa Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA), Profesa William Pallangyo alisema katika mahafali hayo jumla ya wahitimu 1,700 katika kampasi hiyo kati yao wanawake 938 sawa na asilimia 55.2 na wanaume 762 sawa na asilimia 44.8, wamepata tunuku zao kwenye fani mbalimbali.

Alisema jumla ya Wahitimu ngazi ya Cheti cha Awali ni 567, Astashahada 452, Stashahada 491, na Shahada 190.

Profesa Pallangyo alisema idadi hiyo kubwa ya wahitimu wanawake inadhihirisha kwamba TIA inanaunga mkono jitihada za Serikali, kwa kutoa fursa ya mafunzo pasipo ubaguzi.

Alisema idadi ya wahitimu wote wa TIA kwa mwaka wa masomo 2022/2023 kwa Kampasi za Dar es Salaam, Mbeya, Mtwara, Mwanza, Kigoma na Singida ni 13,218 ambapo wanawake ni 7,139 sawa na asilimia 54 na wanaume ni 6,079 sawa na asilimia 46.

Alisema wanaposherehekea mahafali hayo ya Ishirini na moja TIA imepiga hatua kubwa katika uendeshaji wa mafunzo, huduma ya ushauri wa kitaalam, rasilimali watu, pamoja na miundombinu ya kusomea na kufundishia katika kampasi hii ya Singida.

Alisema idadi ya wanachuo wanaodahiliwa katika Kampasi ya Singida imekuwa ikiongezeka mwaka hadi mwaka. Mathalani, katika mwaka huu wa masomo 2023/2024, ulioanza Mwezi Oktoba, 2023, jumla ya wanachuo 1,443 wamedahiliwa katika kampasi ya Singida.

Aliongeza kuwa hata hivyo, zoezi la usajili bado linaendelea na lengo ni kudahili wanachuo wapya 2,600 ukilinganisha na udahili wa wanachuo 1,556 katika mwaka wa masomo 2022/2023. 

Alisema ongezeko hilo la wanafunzi kwa kiasi kikubwa linatokana na mambo makubwa matatu ambayo ni  ubora wa elimu itolewayo inayotokana na mitaala inayowajengea wanachuo wa ngazi zote msingi wa umahiri hivyo kumwezesha mhitimu kuajiriwa na hata kujiajiri pindi anapohitimu masomo yake. Hatua hii huwafanya wazazi na wanafunzi kuichagua TIA.

Utaratibu mzuri wa Serikali wa kuwapangia vyuo moja kwa moja wahitimu wa kidato cha nne waliofaulu na kukidhi vigezo (kupitia TAMISEMI). Mathalan, katika mwaka wa masomo 2023/2024 jumla ya wanafunzi 1,170.

"Ongezeko la mikopo kwa wanafunzi wa kozi za shahada hatua ambayo imewezesha watanzania wengi wenye sifa kumudu gharama za masomo.  Kwa mfano, katika mwaka huu 2023/2024 Serikali imepanga kuwafadhili wanachuo 810 wa shahada katika kampasi hii ya Singida na hili ni ongezeko la asilimia 15.9 ukilinganisha na wanachuo 699 waliofadhiliwa mwaka 2022/2023," alisema Pallangyo.

Mkuu wa Wilaya ya Iramba Suleimani Mwenda akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Singida Peter ambaye alikuwa mgeni rasmi kwenye mahafali hayo alisema amefurahishwa sana na mpango wa ukuzaji na uendelezaji wa wanafunzi kitaaluma na kitaalamu yaani (Career Development Program) wanaoufanya kwa wanafunzi wa taasisi hiyo kwa kujitengenezea fursa muhimu za kibiashara kwa kuendeleza

ubunifu wao ambao ni fursa adhimu kwa wanafunzi hao.

“ Mmedhihirisha umahiri wenu, na kutupa wasaa wa kushuhudia matunda ya juhudi zenu. Hivyo, sina budi kwa niaba ya Serikali, kutoa pongezi zangu za dhati kwa Uongozi, Wahadhiri na wafanyakazi Waendeshaji, kwa kazi nzuri waliyoifanya katika kipindi chote cha mafunzo yenu. 

Safari yenu ya mafunzo haikuwa nyepesi; safari yenu ilihitaji uvumilivu, ushirikiano, nidhamu, kujituma na zaidi ya yote kumtegemea Mungu. Kwa pamoja, haya ndiyo yamewawezesha kufikia hatua hii muhimu,” Mwenda alitoa pongezi hizo kwa niaba ya Serikali.

Aidha, Mwenda aliwaasa wahitimu hao kwamba, hatua

waliyoifikia iwe ni chachu ya kujiimarisha zaidi kitaaluma ili kuweza kushindana katika soko la ajira na kujiajiri na kuwa  Serikali ya Awamu ya sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inahimiza sana Taasisi zote kuhakikisha elimu inayotolewa kwa wanafunzi iwe elimu, ujuzi na maarifa ya kukidhi mahitaji ya soko ili itumike kuleta tija na maendeleo yanayoendana na mabadiliko ya Sayansi na Teknolojia.

 Afisa Mtendaji Mkuu (CEO) wa Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA), Profesa William Pallangyo, akizungumza kwenye mahafali hayo.

Mkurugenzi wa TIA Kampasi ya Singida, Dkt. James Mrema akiwatambulisha wageni waalikwa.


 Mhitimu wa Shahada ya Uhasibu kutoka kampasi ya Singida, Patrick Edward  akipokea cheti kutoka kwa mgeni rasmi 


Viongozi wa TIA wakiwa kwenye mahafali hayo. Kutoka kulia ni Makamu Mkuu wa Chuo, Taaluma, Utafiti na Ushauri wa TIA, Dkt. Momole Kasambala, Makamu Mkuu wa Chuo, Mipango, Fedha na Utawala TIA, Dkt. Issaya Hassanal na Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Masoko TIA, Lilian Rugaitika.

Mratibu wa Taaluma, Flora Lemnge akizungumza. 

Viongozi wakiwa meza kuu. Kutoka kushoto ni Mjumbe wa Bodi ya Ushauri ya Wizara ya Fedha, Thabiti Dokodoko, Mwenyekiti wa Bodi ya Ushauri ya Wizara, Wakili Said Chiguma, Mgeni rasmi wa Mahafali hayo, Mkuu wa Wilaya ya Iramba, Suleiman Mwenda ambaye alimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Singida, Peter Serukamba, Afisa Mtendaji wa TIA, Profesa, William Pallangyo na Mkurugenzi wa TIA, Kampasi ya Singida, Dkt. James Mrema.

Wahitimu wa Shahada ya Usimamizi wa Rasilimali Watu na Utawala wakiwa kwenye maandamano kuelekea kwenye viwanja vya mahafali hayo.



Wahitimu wa Shahada ya Uhasibu wakionesha furaha yao kabla ya kutunukiwa vyeti vyao.

Viongozi mbalimbali na Waadhiri wa TIA wakiwa wamejipanga foleni tayari kwa kumpokea mgeni rasmi wa mahafali hayo.

Mkuu wa Idara ya Mpango wa ukuzaji na Uendelezaji wa Wanafunzi Kitaaluma na Kitaalamu yaani(Career Development Program) wa taasisi hiyo, Imani Matonya (mwenye suti katikati) akiwa katika picha ya pamoja na wajasiriamali wanafunzi wa TIA Kampasi ya Singida wakati wakimsubiri mgeni rasmi kuona bidhaa zao na kuzungumza nao.

Taswira ya mahafali hayo.

Mratibu wa Ujasiriamali na Kituo Atamizi wa Kampasi ya Singida, Mohamed Kaluse, akizungumza kwenye mahafali hayo ya 21.

Wahitimu wa Shahada ya Usimamizi wa Rasilimali Watu na Utawala wakionesha furaha zao baada ya kutunukiwa vyeti vyao.

Waadhiri wa TIA wakiwa kwenye mahafali hayo.