Tuesday, May 9, 2023

TRA SINGIDA YAENDESHA KAMPENI YA TUWAJIBIKE, YATOA ONYO KWA WASIO TOA RISITI ZA KIELEKITRONIKI

Afisa Kodi wa Mamlaka  ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Singida, Hashim Mkwayu akizungumza na mawakala wa mabasi Stendi Kuu ya Mabasi Misuna wakati akitoa elimu kuhusu umuhimu wa  kutoa risiti za kielektroniki kwa abiria wakati wa kampeni maalum iitwayo Tuwajibike ilioanza May 9, 2023 na kuwalenga wafanyabiashara wote.

Na Dotto Mwaibale, Singida. 

MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Singida imeendesha kampeni ya Tuwajibike yenye lengo la kuwataka wafanyabiashara na mawakala wa mabasi kutoa risiti za kielektoniki (EFD) wanapouza bidhaa zao na kuwakatia tiketi abiria wao chini ya kauli mbiu isemayo ukiuza toa risiti na ukinunua dai risiti.

Akizungumza na mawakala wa mabasi Stendi Kuu ya Mabasi Misuna Afisa Kodi wa TRA, Hashim Mkwayu alisema lengo la kampeni hiyo imelenga utoaji wa elimu kwa mawakala wa mabasi kuhusu umuhimu wa  kutoa risiti za kielektroniki kwa abiria na kuwahimiza abiria wao kuhakikisha wanadai risiti tofauti na hapo watatozwa faini.

Alisema TRA mkoani hapa haitasita kuwachukulia hatua kali za kisheria mawakala wa magari ya usafirishaji abiria ambao watabainika kutotoa risiti hizo kwa abiria na abiria ambaye atashindwa kudai risiti.

Alisema adhabu hiyo pia itawahusu mawakala ambao watashindwa kutoa risiti kwa mizigo yote itakayokuwa inasafirishwa kwenye magari hayo.

Alisema kampeni hiyo pia itawahusu wafanyabiashara wote wenye maduka yanayouza bidhaa mbalimbali, maduka ya dawa, vipodozi, chakula, wauza nyama (bucha) mahoteli, nyumba za kulala wageni, vifaa vya ujenzi nguo na nyingine zote.

Aidha, Mkwayu alisema TRA itawachulia hatua mawakala wanaokatisha tiketi katika vituo visivyo rasmi (Vituo Bubu) ambao wanatoa risiti zisizo za kielektroniki kwani kwa kufanya hivyo wamekuwa wakiikosesha Serikali mapato.

Hatua hiyo imekuja kufautia malalamiko kutoka kwa baadhi ya mawakala hao kuhusu kuwepo kwa vituo  bubu ambavyo vinasababisha mkanganyiko wa bei wakati wa kuwaandikia risiti za kielektroniki abiria ambao wameandikiwa tiketi za kawaida na kupelekea kutozwa faini.

Wakala wa mabasi hayo Ibrahimu Abdul alisema vituo hivyo bubu vimekuwa ni changamoto kubwa kwao na akaomba vyombo husika Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA), TRA. Polisi na Manispaa ya Singida wakae pamoja kutafuta njia ya kuiondoa.

" Nia ya Serikali ya ukusanyaji wa mapato ni   njema kwani fedha zinazopatikana ndio zonazotumika kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo, kulipa mishahara, kununua madawa na vifaa tiba na mambo mengine sasa haiwezekani kukawa na watu wachache wanao tuharibia kazi kwa kukwepa kulipa kodi kwa njia za ujanja ujanja," alisema Abdul.

Afisa Elimu kwa Mlipa Kodi kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania TRA Mkoa Singida Swaumu Mvungi alisema mamlaka hiyo itaanza kuyafuatilia maeneo yote ambayo sio rasmi yanayotumika kama vituo vya magari na kutoa risiti ambazo sio za kielekitroniki.

Alivitaja vituo hivyo kuwa ni Sabasaba, Jovena, Namfua na Msufini na akatoa onyo kwa mawakala wanaofanya hivyo kuacha mara moja kabla ya kufikiwa na mkono wa sheria na kuwa kampeni hiyo inafanyika katika wilaya zote mkoani hapa ambazo ni Mkalama, Iramba, Singida Manispaa,Ikungi Manyoni, Itigi na Singida DC..

Mwenyekiti wa Chama cha Mawakala wa Mabasi Mkoa wa Singida, Musafiri Ramadhani alisema jambo la kuondoa vituo bubu hivyo liangaliwe kwa mapana kwani ni changamoto kubwa kwao.

Wakala Patrick Mgimbwa alisema jambo hilo lisifanyiwe masihara wala kufanywa la kisiasa kwani mawakala hao wa vituo bubu wamekuwa wakitoza nauli watoto wa jamii ya kifugaji hadi Sh.50,000 kutoka Singida hadi Dar es Salaam na kuwa wizi huo wa mchana kweupe umepewa jina la 'Abiria zawadi ya Mungu,

Kwa upande wake Wakala Athumani Kimwanga aliwaomba TRA wapite katika maeneo yote vilipo vituo bubu hivyo wakiwa wamevaa nguo za kawaida na kufanya uchunguzi hata kwa kujifanya ni abiria watabaini hayo yanayolalamikiwa na kuweza kuvikomesha vitendo hivyo.

Baadhi ya mawakala wa mabasi Mkoa wa Singida wakipata elimu hiyo iliyokuwa ikitolewa na maafisa wa kodi wa TRA (hawapo pichani)
Maafisa wa TRA waliokuwa kwenye kampeni hiyo. Kutoka kulia ni Victor Mbwambo, Hashim Mkwayu, Benedict Moshi, Swaumu Mvungi na Wilson Bamale.
Maafisa hao wa TRA wakitoa elimu hiyo kwa mfanyabiashara wa duka la vipodozi lililopo maeneo ya  soko kuu mjini hapa.
Afisa Elimu kwa Mlipa Kodi kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA)  Mkoa Singida Swaumu Mvungi akizungumzia kampeni hiyo ambayo ni ya muhimu sana katika kukusanya mapato ya Serikali.
Mwenyekiti wa Chama cha Mawakala wa Mabasi Mkoa wa Singida, Musafiri Ramadhani, akizungumza wakati mawakala hao wakipewa elimu hiyo.
Afisa Kodi wa Mamlaka  ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Singida, Hashim Mkwayu, akibandika nje ya duka kipeperushi kinachozungumzia kampeni hiyo.
Wakala Issa Hussein Nandi akichangia jambo wakati wa kupata elimu hiyo.
Wakala, Ibrahim Abdul akizungumza wakati wa kutolewa kwa elimu hiyo.
Maafisa wa TRA Mkoa wa Singida, wakitoa elimu hiyo kwa mawakala wa mabasi.
Wakala Patrick Mgimbwa akizungumza changamoto waliyonayo kuhusu vituo bubu vinavyotumika kutumika kukatia tiketi abiria kinyume na taratibu.
Wakala Athumani Kimwaga, akichangia jambo wakati elimu hiyo ikitolewa.
 

Sunday, May 7, 2023

SERIKALI KUENDELEA KUSHIRIKIANA NA TAASISI YA TREES FOR THE FUTURE

Mkuu wa Wilaya ya Ikungi, Thomas Apson (katikati waliokaa mbele) akiwa na viongozi wengine, kushoto kwake ni  Mkurugenzi wa Taasisi isiyo ya Kiserikali ya kimataifa ya Trees for the Future Tanzania, Heri Rashid na kulia ni Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi, Ally Mwanga pamoja na wakulima waliohitimu mafunzo ya kilimo mseto yaliyotolewa na Taasisi hiyo. Katika mahafali hayo yaliyofanyika Kata ya Siuyu May 5, 2023 wahitimu hao walitunukiwa vyeti na zawadi mbalimbali. Kushoto walio simama nyuma ni Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi, Haika Masawe na Afisa Tawala wa Wilaya hiyo, Dijovison Ntangeki.

Na Dotto Mwaibale, Singida

SERIKALI imesema itaendelea kushirikiana na Taasisi isiyo ya Kiserikali ya kimataifa ya Trees for the Future Tanzania inayojishughulisha na kilimo mseto, kilimo endelevu kwa wakulima wenye kipato cha chini vijijini ili kutokomeza njaa, Umaskini na Ukataji wa miti, yenye makao yake makuu mkoani Singida  ambayo inatekeleza mradi wa Bustani Misitu.

Hayo yamesemwa na Mkuu wa Mkoa wa Singida, Peter Serukamba katika mahafali ya wakulima 1445 waliohitimu mafunzo ya utekelezaji wa mradi wa Bustani Msitu katika Wilaya ya Ikungi.

"Serikali itaendelea kushirikiana na taasisi ya Trees for future kwani imekuwa na mchango mkubwa wa kusaidia wakulima hapa mkoani kwetu hasa katika uhifadhi wa mazingira na kilimo mseto ambacho kina wasaidiawananchi kupata chakula na mbogamboga" alisema Serukamba.

Aidha, Serukamba aliwataka wananchi mkoani hapa kupanda miti katika maeneo ya kuzunguka nyumba zao na kwenye kingo za barabara na maeneo yote ya taasisi za Serikali ikiwa ni kuunga mkono jitihada za Rais Samia Suluhu Hassan za utunzaji wa mazingira na kuhifadhi vyanzo vya maji.

Mkurugenzi wa taasisi hiyo, Heri Rashid akitoa taarifa kwa mkuu wa mkoa alisema taasisi hiyo imepanda miti ya matunda, mbao, uzio na miti ya kurutubisha udongo na kwamba ifikapo 2030 malengo yao ni kupanda miti bilioni moja.

Alisema miti hiyo ina manufaa makubwa kwa mazingira ikiwa ni pamoja na kufyonza hewa ukaa na kuzalisha hewa safi na inasaidia katika kupambana na mabadiliko ya tabia ya nchi.

Rashid alisema mradi wa Bustani Msitu umekuwa chanzo cha vyakula vya aina mbalimbali vyenye lishe kwa kaya 1445 za wahitimu kupitia upandaji wa mbogamboga na miti ya matunda.

"Wakati tunaanza utekelezaji wa mradi wa Bustani Msitu wanufaika wetu walikuwa chini ya asilimia 25 tu ambao ndio walikuwa na uwezo wa kupata matunda na mbogamboga lakini hivi sasa wanufaika wapo zaidi ya asilimia 83 ambao wanapata mbogamboga na matunda ndani ya saa 48," alisema.

Alisema kupitia mradi huo ambao lengo kuu ni kuongeza uzalishaji katika shamba la mkulima, wakulima wameweza kuuza matunda yao sokoni mjini Singida kama vile pasheni na papai na hivyo kujipatia fedha ambazo zimewasaidia kuendesha maisha yao ya kila siku.

Aliongeza kuwa baada ya wakulima kuanza kunufaika na bustani zao, taasisi ya Trees for the future ilianzisha vikundi 107 vya wakulima vya huduma ndogo za fedha ambavyo vimesajili katika halmashauri za Wilaya ya Singida, Mkalama,Iramba na Ikungi.

Alisema vikundi hivyo vinawasaidia wakulima kuweka akiba na kulipa ili fedha zinazopatikana kutoka kwenye mazao ya Bustani msitu iweze kuzungushwa miongoni mwa wakulima wanufaika hali ambayo imesaidia kuinua hali zo za maisha.

Alisema pamoja na mafanikio yaliyopatikana kumekuwa na changamoto ya tatizo la ukame kutokana na ukanda huu kupata mvua chache, mifugo kuchungiwa kwenye mashamba ya Bustani msitu na upungufu wa fedha za kuendesha miradi.

Mnufaika wa mradi huo Juma Shabani ameishukuru taasisi hiyo kwa kumpa maendeleo katika kilimo hadi kufikia hatua ya kuingiza umeme na maji kwenye nyumba yake aliyoijenga Kata ya Mungaa.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi, Ally Mwanga aliiomba taasisi hiyo kuongeza miaka mingine ya kutekeleza mradi wa namna hiyo kwenye wilaya hiyo ili wananchi wengi waweze kunufaika na teknolojia hiyo ya uhifadhi wa mazingira pamoja na kilimo mseto.

Kabla ya kuanza kwa mahafali hayo RC Serukamba aliyekuwa  ameongozana na kamati ya ulinzi na usalama ya mkoa na wataalam mbalimbali alipata fursa ya kutembea mashamba ya wanufaika wa mradi huo, Basili Mtaturu na Juma Shabani  yaliyopo Kata ya Mungaa na Siuyu ambapo alijionea kazi kubwa iliyofanyika ya utunzaji wa mazingira kupitia kilimo mseto.


Mkuu wa Wilaya ya Ikungi, mkoani Singida,Thomas Apson (katikati) akijiandaa kukata keki maalumu iliyoandaliwa na Taasisi hiyo kwa ajili ya mahafali hayo.
Mkuu wa Mkoa wa Singida, Peter Serukamba akihutubia kwenye mahafali hayo.
Mkurugenzi wa Taasisi hiyo, Heri Rashid akimlisha keki Mkuu wa Wilaya ya Ikungi wakati wa mahafali hayo.
Mratibu wa Shirika hilo Mkoa wa Singida Ibrahim Mghama (kulia) akiongoza msafara wa mkuu wa mkoa wakati ulipotembelea shamba la mnufaika wa mradi huo, Basili Mtaturu wa Kata ya Siuyu. Kutoka kushoto ni Mkurugenzi wa taasisi hiyo, Heri Rashid, Mkuu wa Wilaya ya Ikungi, Thomas Apson, Mnufaikawa mradi huo, Basili Mtaturu na Mkuu wa Mkoa wa Singida, Peter Serukamba.
Muonekano wa kebeji iliyolimwa na mnufaika wa mradi huo, Juma Shabani.
Muonekano wa mapapai katika shamba la mnufaika wa mradi huo Juma Shabani.
Afisa Uhusiano wa Taasisi hiyo Ally Juma, akizungumzia mafanikio makubwa ya mnufaika wa mradi huo, Juma Shabani.
Mnufaika wa mradi huo, Juma Shabani, akiwa shambani kwake.
Msafara wa viongozi mbalimbali ukitoka kutembelea shamba la mnufaika wa mradi huo, Juma Shabani.
Wimbo waTaifa ukiimbwa kwenye mahafali hayo.
Mkurugenzi wa Taasisi ya Trees for the future, Heri Rashid akitoa taarifa ya taasisi hiyo.
Mkuu wa Wilaya ya Ikungi, Thomas Apson akizungumza kwenye mahafali hayo.
Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi, Ally Mwanga (kulia) akiwa naDiwani wa Kata ya Siuyu, Selestine Yunde katika mahafali hayo.
Burudani ya ngoma ya asili ya kabila la Wanyaturu ikitolewa.
Wafanyakazi wa taasisi hiyo wakiserebuka sanjari na wasanii wa Kata ya Siuyu wakati wa mahafali hayo.
Vyeti vikitolewa kwa wakulima wahitimu wa mafunzo ya kilimo mseto yaliyotolewa na taasisi hiyo.
 

Friday, May 5, 2023

MSD YAFANYA MABORESHO UPATIKANAJI BIDHAA ZA AFYA NCHINI

 KatibuTawala  Mkoa wa Singida, Dk.Fatma Mganga akifungua mkutano wa wadau wa Bohari ya Dawa (MSD) uliofanyika Mei 3, 2023 mjini Singida. Kulia ni Meneja wa MSD Kanda ya Kati, John Sipendi na kushoto ni Mganga Mkuu wa Mkoa wa Singida, Dk.Victorina Ludovick. 

Na Dotto Mwaibale, Singida 

BOHARI ya Dawa (MSD) imefanya maboresho katika maeneo mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuingia mikataba ya muda mrefu na wazalishaji ili kurahisisha upatikanaji wa bidhaa za afya nchini. 

Hayo yamesemwa na Meneja wa MSD Kanda ya Kati, John Sipendi wakati akimkaribisha mgeni rasmi KatibuTawala wa Mkoa wa Singida, Dk.Fatma Mganga kufungua mkutano wa wadau wa MSD uliofanyika mjini hapa hivi karibuni na kuhudhuriwa na Mganga Mkuu wa mkoa, Waganga Wakuu wa Wilaya,Wafamasia,Wataalam wa maabara na viongozi wa MSD.

Sipendi alisema ili kufikia dira na kutimiza dhima na malengo yake, MSD inadumisha na kusimamia mfumo wenye tija wa ununuzi, utunzaji na usambazaji wa bidhaa za afya kwa ajili ya vituo vya kutolea huduma za afya vya umma nchini na baadhi ya binafsi vilivyoidhinishwa na Wizara ya Afya. 

Alitaja kazi nyingine ni kutumia ujuzi, weledi, mbinu, taratibu na ushauri wa kitaalamu katika kusimamia na kudhibiti utunzaji na usambazaji wa bidhaa za afya. 

Alitaja eneo lingine ni kufuatilia mahitaji ya bidhaa za afya na kusimamia usambazaji wake katika vituo vya kutolea huduma za afya, huduma za afya katika vituo vya umma na kuboresha pale inapobidi na kuhakikisha upatikanaji wa bidhaa za afya zinapatikana kwa wakati. 

Sipendi aliongeza kuwa ili kuhakikisha hayo  yote yanafanikiwa, MSD imefanya maboresho kwa kukasimu  baadhi ya madaraka na majukumu kwa kanda ili kurahisisha utekelezaji wa majukumu katika eneo hilo.

Aidha, MSD imeanza kusambaza bidhaa za afya mara sita kutoka mara nne ya awali na kuwezesha kuboresha mifumo ya ndani ya utendaji, kuboresha huduma na mawasiliano na wateja.

Alisema kutokana na serikali kutenga na kuleta fedha za kununulia bidhaa za afya kama ilivyopanga, upatikanaji wa bidhaa za afya umepanda kutoka asilimia 54 iliyokuwepo mwishoni mwa mwaka jana na kufikia asilimia 76 sasa, kuongeza wataalamu ili kuweza kuwa na fani mbalimbali kuendana na majukumu ya MSD.

Pia Sipendi alisema MSD imeweza kufanikisha kusambaza vifaa vya uzazi pingamizi wa mama na mtoto (CEmONC), vifaa vya maabara na mashine za kusafisha damu kwa baadhi ya hospitali kama vile Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM).

Naye Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida Dk.Mganga alisema mkutano huo umelenga kuboresha upatikanaji wa dawa na vifaa tiba na kujadili changamoto  zinazovikabili vituo vya afya vya kutolea huduma ili ziweze kupangiwa maazimio na mikakati ambayo itamsaidia mteja au mwananchi kupata huduma iliyo bora. 

“Mheshimiwa Rais wetu Dk.Samia Suluhu Hassan ametoa kipaumbele kikubwa katika sekta ya afya kwa kutoa fedha nyingi za kujenga Hospitali za  Wilaya, Vituo vya Afya na Zahanati , tumejenga majengo ya wagonjwa mahututi (ICU) majengo ya kupata huduma ya dharura ambayo ni ya kisasa,” alisema Dk.Mganga.

Alisema Serikali imefanya yote hayo ili kuwawezesha wananchi kupata huduma bora na za uhakika.

Aidha, Dk.Mganga  alitumia nafasi hiyo kumpongeza Rais Samia kwa kufanya kipengele chake na kilichobakia ni kwa wadau, MSD na wafanyakazi kuboresha pale ambapo amekomea na wanalojukumu la kuhakikisha mgonjwa anapata matibabu bora.

Aliongeza kuwa kumekuwa na malalamiko kutoka kwa baadhi ya wananchi  wanapoambiwa dawa hakuna na jambo ambalo linatokana na madaktari kukalili dawa aina moja wakati magonjwa yaliyo mengi yanatibiwa zaidi ya dawa moja.

"Dawa inaweza kutolewa kama mbadala na kuondoa dhana ya wananchi kuichukia Serikali yao pale wanapoambiwa dawa hakuna, madaktari nawaomba  kabla ya kumuandikia mgonjwa dawa mjue akiba za dawa zilizopo ili kuondoa malalamiko ya wananchi.

Kwa  upande wake Mganga Mkuu wa Mkoa wa Singida, Dk.Victorina Ludovick alisema maagizo yaliyotolewa na Katibu Tawala Mkoa yatafaniwa kazi ikiwamo uboreshaji wa huduma za afya pamoja na upatikanaji wa bidhaa za afya.

Meneja wa MSD Kanda ya Kati, John Sipendi, akizungumza kwenye mkutano huo.

Mfamasia wa Mkoa wa Singida, Elikana Lubango akitoa wasilisho la wateja wa MSD.
Mganga Mkuu wa Wilaya ya Itigi Emmanuel Mallange ambaye alikuwa Mwenyekiti wa mkutano huo akizungumza wakati wa kufunga mkutano huo.
Mfamasia wa Kanda na Afisa Huduma kwa Wateja MSD Kanda ya Kati Dodoma, Michael Mwakuna akichangia jambo kwenye mkutano huo ambapo aliomba wateja wa MSD wawe wanatoa oda siku 10 kabla ili waweze kupata mahitaji yao ya dawa na bidhaa zingine mapema.
Msimamizi wa Huduma za maabara Kanda ya Kati MSD, Omari Hemed Khamis akichangia jambo kwenye mkutano huo
Meneja wa Maabara Hospitali ya Rufaa Mkoa wa Singida, Julius Mwita akizungumza kwenye mkutano huo.
Afisa Mauzo Kanda ya MSD, Dodoma, Innocent Masha akichangia jambo kwenye mkutano huo.
Wadau wa MSD wakiwa kwenye mkutano huo.
Mkutano ukiendelea.
Washiriki wakiwa kwenye mkutano huo.
Mkutano ukiendelea.
Picha ya pamoja na viongozi katika mkutanohuo.
Picha ya pamoja.
Picha ya pamoja. Kutoka kulia waliosimama ni Kaimu Mganga Mkuu wa Wilaya ya Manyoni, Ferdnand Katimwa, Mganga Mkuu wa Wilaya ya Mkalama, Dorisila John, Mganga Mkuu Wiaya ya Ikungi, Solomon Michael, Mganga Mkuu Wilaya ya Iramba, Hussein Sepoko, Mganga Mkuu Wilaya ya Itigi, Emmanuel Mallange, Kaimu Mganga Mkuu Singida Manispaa, Yona Yuna Hamisi na Mganga Mkuu Singida DC, Grace Tongwisangu. 

Thursday, May 4, 2023

TMDA KANDA YA KATI YATOA ELIMU YA MATUMIZI SAHIHI YA DAWA MKOANI SINGIDA

Afisa Mwandamizi Elimu kwa Umma wa Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA), Kanda ya Kati James Ndege, akizungumza na Wanafunzi wa Shule ya Sekondari Dk. Salmin iliyopo Manispaa ya Singida wakati akitoa elimu ya namna bora ya matumizi ya dawa, vifaa tiba na vitendanishi yaliyofanyika leo Mei 4, 2023. 

Na Dotto Mwaibale, Singida

MAMLAKA ya Dawa na Vifaa tiba (TMDA) Kanda ya Kati imetoa elimu ya matumizi sahihi ya dawa, vifaa tiba pamoja na vitendanishi  kwa makundi mbalimbali ya kijamii na wanafunzi Mkoa wa Singida ili kuzuia madhara yanayoweza kutokea kutokana na utumiaji wa dawa hizo kiholela.

Akizungumza na waandishi wa habari wakati wa utoaji wa mafunzo hayo Afisa Mwandamizi Elimu kwa Umma wa TMDA, James Ndege alisema mafunzo hayo yamelenga kutoa elimu hiyo pamoja na kujifunza kutoa taarifa ya madhara yanayotokana na matumizi ya bidhaa hizo.

Alisema matumizi yasiyo sahihi ya dawa na vifaa tiba na vitendanishi yanasababisha athari kubwa kwa watumiaji, watu kupoteza maisha,kupata ulemavu na viungo mbalimbali kuathirika kama ini na , figo.

Ndege alisema elimu hiyo ni muendelezo ili wananchi waweze kujua namna bora ya matumizi ya dawa na ndio maana wameanzisha klabu katika shule mbalimbali ili elimu hiyo inayotolewa na TMDA iweze kusambaa kila maeneo na kuifanya jamii kuelewa athari za matumizi ya dawa hizo.

Aidha Ndege alitoa wito  kwa wananchi kuzingatia matumizi sahihi ya dawa ikiwemo kuepuka matumizi holela ya dawa kwa kutumia dozi kikamilifu sambamba na kupata vipimo na ushauri wa wataalam wa Afya kabla ya kutumia dawa hizo.

Alisema kuna changamoto kubwa kwenye jamii ya watanzania kwani baadhi yao wamekuwa wakitumia  dawa wanapojisikia kuumwa bila kupima wala kupata ushauri wa daktari na kwamba wengi wao zimewapelekea kupata madhara kiafya.

"Kuna changamoto kubwa katika jamii kwa watu kutumia dawa kiholela na sisi TMDA tunaendelea kuwaelimisha kuwa utumiaji wa dawa kiholela unaweza kusababisha usugu wa bakteria na kufanya dawa hizo kushindwa kufanyakazi kama inavyotakiwa" alisema Ndege.

Pia Ndege aliwataka wananchi kuzingatia muda wa kutumia dawa hizo kama walivyoelekezwa na madaktari kwani kutumia dawa hizo kwa muda ambao hawajaelezwa zinaweza kuwaletea changamoto za kiafya.

Aidha alitoa angalizo kwa wanafunzi wasichana kuacha ama kutojiingiza katika matumizi ya dawa za dharura za kuzuia mimba hasa katika wakati huu ambao wapo shuleni na umri mdogo na kuwa matumizi ya dawa hizo zinaweza kuwa na athari kubwa kwao za mfumo wa uzazi pindi wakiwa watu wazima na umri unaoruhusiwa kufunga ndoa au kupata watoto.

Ndege pia alitoa angalizo hilo kwa wanafunzi wavulana nao kuacha kutumia dawa za kuongeza nguvu za kiume ambapo nao wanaweza kupata athari zilezile ambazo zinaweza kuwapata wasichana na badala yake aliwataka kusoma kwa bidii na kufanya mazoezi hali itakayowasaidia kutowaza kufanya ngono.

Katika mafunzo hayo waliweza kuzindua klabu zilizoanzishwa na TMDA katika shule mbali kwa ajili ya kutoa elimu kuhusu matumizi yasiyo sahihi ya dawa, vifaa tiba na vitendanishi na masuala yote yasiyo salama ya matumizi ya dawa hizo.

Shule ambazo zimepatiwa mafunzo hayo hadi leo May 4, 2023 ni shule sita za sekondari za Kindai, Dk. Salmin, Ipembe, Senge Singida, Utemini na wananchi wa Kata za Mitunduruni, Majengo na Mungumaji zote za Manispaa ya Singida..

Mkaguzi wa Dawa Kanda ya Kati, Saraphina  Cleophace akizungumza na wanafunzi hao wakati akijibu maswali mbalimbali.
Mkuu wa Shule ya Sekondari  Dk.Salmin, Juma Thomas akielekeza jambo wakati wa mafunzo hayo.
Mkaguzi wa Dawa Kanda ya Kati, Saraphina  Cleophace, akimkabidhi vipeperushi Mkuu wa shule hiyo, Juma Thomas vitakavyotumika kuwafundishia wanafunzi.
Picha ya pamoja na wanachama wa Klabu ya TMDA Shule ya Sekondari ya Kindai.
Mlezi wa Klabu ya TMDA Mwalimu Alimas Jumanne Alimas wa Shule ya Sekondari ya Kindai akipokea vipeperushi vya kujifunzia kutoka kwa Mkaguzi wa Dawa Kanda ya Kati, Saraphina  Cleophace,
Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Dk.Salmin, Mwalimu Juma Thomas akizungumza na wanafunzi.
Wanafunzi wakipata mafunzo hayo.
Mafunzo yakiendelea.
Afisa Mtendaji wa Kata Mughanga, akizungumza na wananchi wa Kata hiyo (hawapo pichani) kabla ya kupata elimu hiyo.
Wananchi wa Kata ya Mughanga wakiwa kwenye mafunzo hayo.
Mafunzo yakiendelea.