Thursday, February 4, 2021

WANAMUZIKI ZAIDI YA 500 KUHUDHURIA KONGAMANO LA FURSA JIJINI ARUSHA

Waziri wa Habari, Sanaa na Michezo, Innocent Bashungwa ambaye anatarajiwa kuwa mgeni rasmi kwenye kongamano la fursa la wanamuziki litakalofanyika Februari 20 jijini Arusha.

Mwanamuziki mkongwe hapa nchini, Kida Waziri atakabidhiwa kadi ya matibabu ya NHIF kwenye kongamano hilo.
Wanamuziki Madamu Flora (kulia) na Stellah Joel watakuwepo kwenye kongamano hilo.

Mwanamuziki Emmanuel Mbasha atakuwepo kwenye kongamano hilo.


Mwanamuziki Goodluck Gozibeth atakuwepo kwenye kongamano hilo.
Mwanamuziki Mabisa atakuwepo kwenye kongamano hilo.
 


Na Dotto Mwaibale.


WANAMUZIKI zaidi ya 500 kutoka kada mbalimbali nchini wanatarajia kuhudhuria kongamano la fursa litakalofanyika Februari 20 jijini Arusha.

Katika kongamano hilo baadhi ya wanamuziki hao watakabidhiwa kadi za bima ya afya ya Taifa (NHIF) na Waziri wa Habari, Sanaa na Michezo, Innocent Bashungwa ambaye anatarajiwa kuwa mgeni rasmi.

  "Wanamuziki watakao pata kadi hizo ni wale ambao wametimiza vigezo kama walivyoeleza Rais wa Umoja wa Wanamuziki Tanzania (TAMUFO), Eric Kisanga na Katibu Mkuu wa umoja huo, Stella Joel ambao ndiyo waandaaji wa kongamano hilo.

Baadhi ya wanamuziki watakao kabidhiwa kadi hizo wametajwa kuwa ni mwanamuziki mkongwe hapa nchini, Kida Waziri,  Emmanuel Mbasha, Madamu Flora, Goodluck Gozibeth, Stara Thomas, Hafsa Kazinja Renatha Sedekia na Rehema Tajiri.

Akiwazungumzia Wanamuziki hao Katibu Mkuu wa TAMiUFO Stella Joel alisema wanaishukuru Serikali kwa kuwakumbuka kuwapatia kadi hizo ambazo zitawasaidia kupata vipimo na matibabu katika hospitali za Serikali na binafsi.

Joel alisema kabla ya hapo wanamuziki wengi wamekuwa wakipoteza maisha kwa kushindwa kumudu gharama za vipimo na matibabu.

" Kwa hatua hii iliyochukuliwa na Serikali ya awamu ya tano hakika wanamuziki wote tunakila sababu ya kuipongeza  kwa kutekeleza ahadi yake kwa vitendo ya kutusaidia wasanii" alisema Joel.

Rais wa TAMUFO,  Eric Kisanga alisema kongamano hilo ni la kipekee kwani litawahusisha wanamuziki wa kada zote  na kuwa maandalizi yote yamekwisha kamilika.

" Maandalizi yote ya kongamano letu ili la fursa kwa wanamuziki yamekwisha kamilika kwa asilimia kubwa na sasa tupo kumalizia mambo madogo yaliyosalia" alisema Kisanga.

Kisanga alitumia fursa hiyo kuwakaribisha wananchi na wadau wengine kwenye kongamano hilo. 


No comments:

Post a Comment